9: Kushindwa Ghafla kwa Figo

Ugonjwa wa figo wa muda

Ugonjwa huu wa figo wa muda ni upi ?

Katika ugonjwa huu kupungua au kukoma kwa kazi ya figo hutokea kwa muda mfupi wa saa,siku au hata wiki kadhaa. Hii si hali ya kudumu na huweza kutibika au kurudi katika hali yake ya awali.

Chanzo cha ugonjwa huu ni nini ?

Kuna sababu kadha za hali hii. Sababu muhimu ni kama

  1. Kupungua kwa damu kwenye figo;upungufu wa maji mwilini kwa sababu ya kuhara, kupoteza damu nyingi, kuungua moto au kupungua kwa shinikizo au kasi ya damu kwa sababu tofauti tofauti.
  2. Maambukizo makali, ugonjwa mkali au kufuatia upasuaji mkubwa.
  3. Kuziba ghafla kwa njia ya mfumo wa mkojo; jiwe la figo ndiyo mara nyingi husababisha njia ya mkojo kuzibika.
  4. Sababu nyingine muhimu ni; ugonjwa wa malaria (falciparum malaria), leptospirasis, kuumwa na nyoka, magonjwa fulani ya figo, ujauzito, matatizo na athari za dawa fulani kama zile za kutuliza maumivu kama aspirin,brufen au zinazotibu maambukizo kama vile erythromycin.

Dalili za ugonjwa wa figo wa muda

Katika ugonjwa huu kazi ya figo hudhoofika katika muda mfupi na uchafu huongezeka mwilini. Hii huleta athari katika usawa ufaao wa maji na electrolaiti mwilini. Kwa sababu tatizo la ugonjwa wa figo wa muda hutokea ghafla, mgonjwa hupata dalili kali na mapema.Aina ya dalili hizi na ukali wake hutofautiana kati ya mgonjwa na mgonjwa.Dalili zinazosababisha tatizo hili mara nyingi ni:

  1. Magonjwa yaliyo sababisha kufeli kwa figo, ni kama kuhara,kupoteza damu nyingi,homa au baridi.
  2. Kupungua kwa mkojo ingawa kwa wagonjwa wengine hubaki kawaida . Kuongezeka kwa maji mwilini husababisha kuvimba kwa vifundo vya miguu, miguu na kuongezeka kwa uzito.
  3. Kukosa hamu ya chakula, kichefuchefu, kutapika, kuwa na kwikwi, uchovu na hata kuchanganyikiwa.
  4. Dalili za hatari kama kushindwa kupumua, maumivu kwenye kifua,kuzimia,kutapika damu au kuwa na mapigo ya moyo yasiyo ya kawaida kwa sababu ya kuongezeka kwa potasiamu mwilini.
  5. Mapema katika ugonjwa huu wagonjwa wengi huwa hawaonyeshi dalili zozote na ugonjwa hujulikana tu kwa bahati wakati mtu anapimwa kwa sababu nyingine.
Ugonjwa Wa Figo Wa Muda Huja Ghafla Na Mara Nyingi Hubainishwa Na Figo Kutokufanya Kazi Kwa Muda.

Kutambua

Kutambua ugonjwa wa figo wa muda

Wagonjwa wengi walio na hali hii hukosa dalili dhahiri za ugonjwa huu na wakati mwingine hukosa dalili zozote.Kwa hiyo iwapo mtu ana ugonjwa unaoweza kusababisha hali hii ya figo, au iwapo kuna shaka kuhusu dalili fulani fulani, ni lazima uchunguzi wa figo ufanywe mara moja.Kufeli kwa figo huthibitishwa tu kwa vipimo vya damu vinavyoonyesha uwepo wa kreatinini ya damu na yurea vimeongezeka, kiasi cha mkojo na picha za ultrasound kwa wagonjwa walio na historia ya ugonjwa au kufeli kwa figo kwa muda kuonyesha dalili za ugonjwa huu, vipimo na uchunguzi mbalimbali hufanywa ili kujua chanzo cha ugonjwa, matatizo yanayoambatana na hali hii (complications) na pia kuona kama kuna athari nyigine kwa ugonjwa huu.

Ugonjwa wa figo wa muda hupona kabisa matibabu mwafaka yakizingatiwa.

Matibabu

Matibabu ya ugonjwa wa figo wa muda.

Kwa wagonjwa wengi matibabu sahihi yakizingatiwa,ugonjwa huu hupona kabisa. Kukawia au matibabu yasiyofaa kwa ugonjwa huu huhatarisha maisha.

Hatua kuu aa kukabiliana na ugonjwa wa figo wa muda ni

  1. Kutibu chanzo au sababu za ugonjwa huu.
  2. Matibabu ya dawa na hatua nyiingine zitakazo saidia.
  3. Ushauri kuhusiana na vyakula.
  4. Dayalisisi (kazi ya figo kufanywa na mashine).

1. Kutibu chanzo cha ugonjwa wa figo

  • Kutambua na kutibu hali yoyote iliyosababisha kufeli kwa figo ndiyo hatua muhimu sana ya kukabiliana na ugonjwa huu.
  • Matibabu sahihi ya chanzo kama shinikizo la damu, maambukizi,kuziba kwa njia ya mfumo wa mkojo nk ni muhimu iwapo tunataka figo zitapone.
  • Matibabu haya huhakikisha kuwa madhara zaidi hayafanyiki na hivyo kuzipa nafasi figo kupona.
  • 2. Matibabu ya dawa na hatua zinazozingatiwa
  • Lengo hapa ni kusaidia figo na kuzuia au kutibu matatizo yoyote.
  • Kutibu maambukizi na kuzuia dawa zozote ambazo zinaweza kudhuru figo.
  • Kutumia dawa kama frusemide ambazo husaidia kutoa mkojo ili kuzuia mwili kuvimba na mgonjwa kushindwa kupumua.
  • Hatua zingine ni kama dawa za kudhibiti shinikizo la damu, kuzuia kutapika, kushindwa kupumua, kuzimia na pia kupunguza kiwango cha madini ya potasiamu mwilini.
Katika ugonjwa wa figo wa muda,matibabu ya mapema na yanayofaa husaidia figo kupona bila dayalisisi.

3. Ushauri wa vyakula

  • Kuzingatia vyakula vinavyofaa huzuia au hupunguza dalili za figo kufeli.
  • Kuzingatia kiasi gani cha kunywa kulingana na vipimo vya mkojo ili kuzuia kuvimba mwili na matatizo mengine kama kushindwa kupumua.
  • Kuzuia vyakula vyenye potasiamu kama vile matunda,maji ya matunda,matunda makavu-ili kuzuia potasiamu kuwa nyingi kwenye damu,hali ambayo huambatana na figo kufeli na huwa hatari sana kwa maisha.
  • Kuzuia chumvi ili kuzuia kuvimba mwili na matatizo mengine kama yale ya shinikizo la damu na kushindwa kupumua.
  • Lishe bora na ya kutosha ni muhimu.

4. Dayalisisi

Kazi ya figo kufanywa kwa mashine kunaweza kuhitajika kwa wagonjwa wengine tatizo la figo kufeli ghafla hadi wakati figo itakapopona.

Dayalisisi ni nini?

Dayalisisi ni njia mbadala ya kufanya kazi za figo kwa kutumia mashine.Husaidia kudumisha uhai kwa watu ambao figo zao zimefeli kabisa. Kazi muhimu za figo huwa ni kutoa maji yasiyohitajika na kusawazisha asidi na vitu vingine mwilini. Kuna aina mbili za dayalisisi: dayalisisi ya damu na dayalisisi ya tumbo.

Mahitaji ya dayalisisi ni ya siku chache tu lakini kuchelewesha ni hatari kwa maisha.

Kuzuia

Dayalisisi huhitajika lini katika ugonjwa wa figo wa muda?

Dayalisisi huhitajika kwa wagonjwa fulani wenye ugonjwa huu uliozidi,yaani, dalili na matatizo yake yanaendelea kuongezeka licha ya matibabu ya msingi na sahihi. Dayalisisi hudumisha uhai na afya njema hata kama figo zimefeli. Maji huzidi mwilini, ongezeko kubwa la potasiamu na asidi, ni ishara kuu kuwa dayalisisi inahitajika.

Dayalisisi huhitajika kwa muda gani kama figo zimefeli ghafla?

  • Wagonjwa wengine huhitaji dayalisisi kwa muda mfupi tu hadi figo zitakaporudia kufanya kazi zake.
  • Wagonjwa hupona, kwa kawaida, baada ya wiki moja hadi nne, wakati huo dayalisisi huitajika kufanya kazi badala ya figo.
  • Iwapo dayalisisi imefanywa kwa mtu mara moja, haina maana kuwa mtu huyo atahitaji dayalisisi maisha yake yote. Haya ni mawazo potofu. Kuchelewesha dayalisisi kwa sababu tu ya kuogopa kuihitajika maisha yote, kunaweza kuhatarisha maisha ya mgonjwa mwenye figo iliyo feli.

Kuzuia ugonjwa wa figo wa muda

  • Matibabu ya mapema ya vyanzo vya ugonjwa huu na uchuguzi wa mara kwa mara kwa watu waliopata ugonjwa huu.
  • Kuzuia msukumo wa chini wa damu(hypotension) na kutibu hali hii mara tu itambulikapo /inapotokea.
  • Kutotumia dawa zinazoweza kudhuru figo na kutibu maambukizi na kupungua kwa mkojo haraka.