23: Maambukizi ya Mfumo wa Mkojo kwa Watoto

Maambukizi ya Mfumo wa Mkojo Kwa Watoto

Maambukizo ya njia ya mkojo ni tatizo la kawaida kwa watoto wanalokuwa nalo. Shida hii inaweza kuwa ya muda mfupi au ya muda mrefu.

Kwa nini maambukizo ya njia ya mkojo kwa watoto huhitaji matibabu ya haraka kuliko kwa watu wazima?

Maambukizo ya njia ya mkojo huitaji matibabu ya haraka na mara moja kwa sababu:

  • Huwapa homa kwa watoto .Haya ndiyo maambukizo ya tatu ambayo huwapata watoto kwa wingi ikiwa pamoja na ya kifua na kuharisha.
  • Kuchelewesha matibabu au kutolewa matibabu yasiyofaa ni hatari kwani yanaweza kuleta madhara ya kudumu kwenye figo.Ugonjwa huu unaporudia rudia husababisha makovu kwenye figo ambayo yanaweza kuleta shinikizo la damu,figo kutokukua na hata ugonjwa sugu wa figo.
  • Kwa sababu ya dalili zake zisizo wazi, Maambukizo ya njia ya mkojo mara nyingi hayatambuliki na mara nyingi hayafikiriwi, kwa hiyo lazima uchunguzi wa kina ufanywe ili shida ibainike.
  • Ugonjwa huu huwa na hatari ya kurudi tena na tena.

Ni mambo yapi humfanya mtoto awe katika hatari ya kuupata ugonjwa huu?

  • Maambukizo ya njia ya mkojo huwapata wasichana mara nyingi zaidi kwa sababu njia yao ya mkojo ya yurethra ni fupi.
  • Wasichana kujipanguza kutoka nyuma kuelekea mbele ( badala ya kutoka mbele kwenda nyuma) baada ya kwenda choo.
  • Watoto wenye shida za kimaumbile kama mkojo unaorudi nyuma kutoka kwa kibofu hadi kwenye yureta na kuelekea kwenye figo,au njia ya mkojo iliyo upande wa nyuma.(posterior urethral valve)huwa na hatari zaidi ya maambukizo.
  • Wavulana ambao hawajatahiriwa wamo hatarini zaidi ya kupata maambukizo kuliko wale waliotahiriwa.
  • Kuwa na jiwe kwenye mfumo wa mkojo.
  • Sababu zingine; kufunga choo, kushindwa kuondoa uchafu sehemu ya siri (poor perineal hygiene), kuwekwa tyubu ya katheta kwa muda mrefu na historia ya maambukizo haya katika familia.
Maambukizo ya njia ya mkojo ni chanzo cha kuleta homa kwa watoto.

Dalili

Dalili za maambukizo ya njia ya mkojo

Watoto wakubwa kidogo wanaweza kusema shida yao.Dalili kwa watoto kama hawa huwa kama zile za watu wazima.(Angalia sura ya kumi na nane).

Watoto wa umri mdogo hawawezi kusema / kulalamika. Kulia wanapo kojoa, mkojo wenye harufu mbaya na homa ni dalili za maambukizo. Watoto wadogo pia hukosa hamu ya chakula, hutapika au kuhara, kutoongeza uzito vizuri, hukonda,wepesi wa hasira na wakati mwingine hakuna dalili zozote.

Dalili za kawaida za maambukizi kwenye mfumo wa mkojo kwa watoto ni homa za kujirudia rudia, kutokuongezeka uzito na matatizo ya mkojo.

Utambuzi

 

Utambuzi wa maambukizo ya njia ya mkojo

Uchunguzi ufanywao kwa watoto ni:
1. Uchunguzi wa msingi

  • Mkojo hupimwa kama ilivyoelezwa katika sura ya kumi na nane(microscopy na dipstick).
  • Kuchunguza mkojo kwa njia maalum ili kudhibitisha aina ya viini vya bacteria vinavyohusika na kuamua dawa bora za antibayotiki zitakazotumiwa.
  • Kupimwa damu, yurea, umajimaji wa kreatinini, sukari na protini na vinginevyo kama C reactive protein, hemoglobin, WBC jumla na aina mbalimbali.

2. Uchunguzi ili kutambua hali za hatari zinazoambatana na maaambukizo

  • Kupigwa picha ili kujua kasoro zilizopo katika figo na kibofu, eksirei ya tumbo, picha ya njia ya mkojo.Kuona kiasi gani cha mkojo kinabaki – VCUG,CT Scan or MRI ya tumbo na IVU(intravenousurography).
  • Uchunguzi ili kujua iwapo figo lina/zina makovu.Uchunguzi huu ni muhimu hufanyike miezi mitatu hadi sita baada ya ugonjwa.
  • Uchunguzi ili kujua uwezo wa kibofu wa kufanya kazi.

Uchunguzi wa maumbile ya mfumo wa njia ya mkojo. Lini na ufanyikeje

  • VCUG: Uchunguzi huu wa eksirei ni muhimu sana kwa watoto wenye maambukizo na wenye kasoro ya mkojo kurudi nyuma.
  • VCUG pia ndio uchunguzi unaowezesha kutambua kasoro ya mkojo kurudi nyuma na kiasi cha kasoro hii, pia huweza kutambua kasoro za kimaumbile za kibofu au/na yurethra.
  • Uchunguzi wa VCUG ufanyike kwa kila mtoto mwenye umri wa chini ya miaka miwili baada ya maambukizo ya kwanza ya UTI.
  • Uchunguzi unafaa ufanyike baada ya kutibu maambukizo, wiki moja baada ya ugonjwa kutambulika.
  • Katika uchunguzi huu kibofu hujazwa maji maalum yenye rangi inayoonekana kwenye eksrei. Katheta hutumika na usafi kuzingatiwa.pia mgonjwa hupatiwa dawa za antibayotiki kabla ya kipimo.
  • Picha za eksirei hupigwa kabla ya rangi kujazwa, uchunguzi huu huwezesha kuona maumbile na jinsi kibofu na yurethra zinavyofanya kazi.
  • Uchunguzi huu (VCUG) huweza kuonyesha mtiririko wa mkojo kutoka kwenye kibofu kama utarudi nyuma hadi kwenye yureta au kwenye figo. Pia kipimo hiki huwa ni muhimu katika kutambua kama njia ya mkojo inayofungukia upande wa nyuma, kwa watoto wachanga wanaume.
Vipimo muhimu sana kwa utambuzi vitu vinavyoleta maambukizi kwenye mfumo wa mkojo ni ultrasound, VCUG na IVU.

Kuzuia

Kuzuia maambukizo ya njia ya mkojo

  1. Kunywa maji mengi.Maji huzimua mkojo na huwezesha kutoa bacteria kwenye kibofu na njia ya mkojo.
  2. Mtoto inafaa akojoe kila baada ya saa mbili au tatu.Kuweka mkojo kwa muda mrefu huwapa bacteria nafasi ya kukua.
  3. Sehemu za siri za mtoto ziwe safi wakati wote.Mpanguze mtoto kutoka mbele ukielekea nyuma,na si nyuma hadi mbele.Hii huzuia bacteria kutoka kwenye tupu ya nyuma ambayo huwa na choo kuingia kwenye yurethra.
  4. Mbadilishe mtoto mara tu aendapo choo ili kuzuia kinyesi kugusa sehemu za mbele.
  5. Mtoto avishwe nguo za ndani za pamba tu ili kuwezesha upepo kuzunguka.Usimvishe mtoto nguo za ndani zilizomkaza au za nailoni.
  6. Kwa mvulana ambaye hajatahiriwa, ngozi ya mbele ya uume wake inafaa kuoshwa kila anapoogeshwa au mara nyingi zaidi.
  7. Mtoto mwenye VUR inafaa ajaribu kukojoa muda mfupi tu baada ya kumaliza kukojoa ili kuhakikkisha mkojo haubaki kwenye kibofu.
  8. Kwa watoto ambao wamo hatarini kupata maambukizo, dozi ya kiwango cha chini ya antibayotiki inafaa kutumiwa kila siku kuzuia maambukizo.
VCUG ni kipimo cha x ray muhimu sana kinachotumika kwa watoto wenye maambukizi ya mfumo wa mkojo kujua iwapo valvu za urethra zimeathirika. (vesicoureteral reflux na posterior urethral valve).

Matibabu

Matibabu ya maambukizo ya njia ya mkojo

Hatua za jumla

  • Mtoto afunzwe kuzingatia hatua zote za kuzuia maambukizo.
  • Mtoto mwenye maambukizo anywe maji mengi.Iwapo amelazwa hospitalini basi huwekewa maji kupitia kwenye mshipa.
  • Dawa zifaazo zinafaa kutumiwa kupunguza joto/homa.
  • Baada ya matibabu ni muhimu mkojo upimwe ili kuhakikisha kuwa maambukizo yameisha.Baada ya hapo, ni muhimu mkojo upimwe mara kwa mara ili kuhakikisha kuwa maambukizo hayarudi.
  • Watoto wote wenye maambukizo wafanyiwe uchunguzi wa kina hasa ule wa picha(ultrasound).

Matibabu Maalumu

  • Kwa watoto, maambukizo yatibiwe haraka kwa dawa za antibayotiki ili kulinda figo zao zinazokua.
  • Mkojo uchunguzwe kabla ya kuanza matibabu ili kujua dawa za antibayotiki zinazofaa kutumiwa.
  • Mtoto anahitaji kulazwa hospitalini na kupewa dawa kupitia mshipa iwapo ana homa kali, anatapika, ana maumivu ya upande mmoja au zote za tumbo au iwapo hawezi kumeza dawa.
  • Antibayotiki za kumeza hupatiwa watoto walio na umri wa kati ya miezi mitatu hadi miezi sita, na ambao si wagonjwa sana na wanaweza kumeza dawa.
  • Dawa za antibayotiki hutumiwa kwa siku saba hadi kumi na nne.Ni muhimu mtoto apatiwe dawa mapema na azimalize. Usiache kumpatia dawa hata kama dalili za maambukizi zimeisha.

Maambukizo yanayojirudia tena na tena

Watoto wenye maambukizo yanayojirudia tena na tena huhitaji kupigwa picha ili kujua chanzo cha maambukizo.Sababu tatu ambazo zinaweza kutibiwa ni mkojo unaorudi nyuma, yurethra inayofungukia upande wa nyuma na mawe ya figo. Kutegemea chanzo cha maambukizo, matibabu sahihi pamoja na hatua za kuzuia maambukizo na dawa za antibayotiki kwa muda mrefu hupangwa.Aidha kwa watoto wengine,upasuaji hupangwa na daktari bingwa wa figo na daktari bingwa wa mfumo wa mkojo(nephrologist na urologist).

Yurethra inayofungukia upande wa nyuma huziba upande wa chini wa njia ya mkojo kwa wavulana na huleta ugonjwa sugu wa figo hali hii isipotibiwa mapema.

Yurethra inayofungukia upande wa nyuma

Yurethra inayofungukia upande wa nyuma

Kasoro hii ya kimaumbile hutokea kwa wavulana.Hii ndiyo sababu kuu ya njia ya mkojo kuziba upande wa yurethra chini.

Shida na umuhimu wake:

Nyama iliyojikunja ndani ya yurethra husababisha kuziba kiasi au kuziba kabisa kwa mtiririko wa mkojo.Njia ya mkojo kuziba husababisha kibofu kufinyika. Kibofu hupanuka sana na ngozi ya msuli ya kibofu huwa nzito/nene. Kibofu kilichotanuka sana na mkojo kujaa na hupelekea mkojo kupanda kwenye ureta na hatimae kwenye figo. Hii husababisha yureta na kibofu kupanuka. Kupanuka huku kusiporekebishwa haraka kunaweza kuleta ugonjwa sugu wa figo. Kama asilimia ishirini na tano (25%) hadi thelathini (30%) ya watoto wanaozaliwa na hali hii figo hufeli. (ESKD) Kwa hiyohali hii ni sababu kubwa ya ugonjwa na vifo kwa watoto.

Dalili

Mtiririko hafifu wa mkojo, mkojo kudondoka, ugumu wa kukojoa, kukojoa kitandani, upande wa chini wa tumbo kujaa kwa sababu ya kibofu kuwa kikubwa na maambukizo.

Peleka mkojokwa ajili ya kuotesha bacteria na kuona dawa inayofaa. Haya yafanyike kabla ya kuchagua /kuanza dawa ya antibiotiki.

Utambuzi

Kupigwa picha (Ultrasound) kabla ya kuzaliwa au baada tu ya kuzaliwa ndiyo njia ya kwanza ya kutambua kuwa mtoto wa kiume ana shida hii (PUV). Hali hii.hudhibitishwa kwa kipimo kinachotumia maji yenye rangi na picha za eksirei hufanywa baada tu ya mtoto kuzaliwa.

Matibabu

Madaktari bingwa wa upasuaji wa figo na wa njia ya mkojo hutibu hali hii kwa pamoja.(Urologist na nephrologist). Matibabu ya kwanza kabisa ni kuingiza tyubu ya katheta kwenye kibofu kupitia kwenye yurethra au kwenye tumbo (karibu na kinena – supra pubic), ili kumimina mkojo. Wakati huo huo matibabu ya maambukizo, anemia au kufeli kwa figo, lishe bora na kurekebisha kiwango cha maji yanayohitajika mwilini na electrolaites husaidia katika kuleta nafuu ya hali ya mgonjwa.

Matibabu halisi ya yurethra iliyofungukia upande wa nyuma ni upasuaji ambao hufuata baada ya hatua za kusaidia hali hii. Kuziba huondolewa na daktari mpasuaji kwa kutumia mashine maalumu (Endoscope).Watoto wote huhitaji kumwona daktari mara kwa mara kwa maisha yao yote kwa sababu ya hatari ya maambukizo ya njia ya mkojo, kutokukua vizuri, kasoro za maji ya mwili, anemia, shinikizo la damu na ugonjwa sugu wafigo (CKD).

PUV huleta kizuizi cha mkojo kwenye sehemu ya chini ya mfumo wa mkojo na inaweza kuleta CKD kama haikutibiwa kwa wakati.

Kasoro ya mkojo kurudi nyuma

Kasoro ya mkojo kurudi nyuma

Mkojo hurudi nyuma kutoka kwenye kibofu hadi kwenye yureta.

Mambo muhimu ya kujua kuhusu hali hii

Hali hii hupatikana kwa asilimia thelathini hadi arobaini ya watoto wenye maambukizo ya njia ya mkojo yanayoambatana na homa. Kwa watoto wengi hali hii husababisha makovu na uharibifu wa figo. Kovu kwenye figo huweza kuleta shinikizo la damu, matatizo kwa wasichana/akina mama wenye mimba hata kusababisha kifafa cha mimba, ugonjwa sugu wa figo na hata figo kufeli (ESKD). .Hali ya mkojo kurudi nyuma mara nyingi huathiri watoto wa mtu mwenye hali hii na mara nyingi wasichana.

Nini maana ya mkojo kurudi nyuma na kwa nini hali hii hutokea

Kasoro hii ya mkojo kurudi nyuma kutoka kwenye kibofu hadi kwenye ureta na hata kwenye figo inaweza kutokea upande mmoja au hata pande zote mbili za mfumo wa mkojo. Kwa kawaida mkojo huteremka kutoka kwenye figo hadi kwenye kibofu kupitia kwenye yureta.

Wakati wa kukojoa kibofu kikijaa mkojo, kuna kilango kati ya kibofu na yureta ambacho huzuia mkojo kurudi nyuma.Mkojo hurudi nyuma wakati kilango hiki kikiwa na kasoro.Hali hii hupimwa kulingana na mkojo kurudi nyuma. Kiasi cha mkojo kinaweza kuwa kidogo au kingi na kwa hiyo uwekewa daraja. (gredi ya kwanza hadi ya nne).

Nini husababisha mkojo kurudi nyuma?

Kuna aina mbili ya hali hii: Hali ya Msingi ambayo hupatikana sana, ni mtoto huzaliwa nayo. Aina ya pili hutokea wakati wowote na husababishwa na kilango au kibofu kuwa na kasoro au maambukizo ya kibofu au yurethra.

Dalili za mkojo kurudi nyuma

Hakuna dalili halisi za hali hii lakini maambukizo ya njia ya mkojo ya mara kwa mara yanaweza kuwa ishara yake. Kwa watoto wa umri mkubwa kidogo wenye hali hii, dalili huwa dhahiri kwa sababu ya matatizo kama shinikizo la damu, protini kwenye mkojo au figo kushindwa kufanya kazi.

Utambuzi

Mtoto akishukiwa kuwa na hali hii, uchunguzi ufuatao hufanywe:.

1. Uchunguzi wa msingi

  • Maji yenye rangi huwekwa kupitia kwenye yurethra au tumbo na picha za eksirei kupigwa.
  • Hali hii hupimwa kuwa ni kidogo au kubwa kulingana na kiasi cha mkojo unaorudi. Hii huwa kipimo muhimu cha kujua hali na jinsi ya kutibu shida hii.
Matumizi yaantibiotiki mara kwa mara na kwa muda mrefu(Kwa miaka),shida ya mkojo kurudi kidogo kidogo inaweza kuondoka bila kupasuliwa.

  • Ikiwa ni kiasi kidogo cha mkojo hurudi kwenye yureta(gredi ya kwanza na ya pili )Na ikiwa hali hii ni kubwa, mkojo mwingi hurudi na yureta kupanuka na pia kibofu kuvimba sana(gredi tano)

2. Uchunguzi zaidi

  • Mkojo kupimwa ili kujua iwapo kuna maambukizo.
  • Damu hupimwa himoglobini, chembechembe nyeupe za damu na umajimaji wa kreatinini.
  • Figo na kibofu kupigwa picha za ultrasound ili kujua ukubwa na maumbo ya figo na iwapo kuna makovu, mawe, kuziba au kasoro nyingine. Picha haziwezi kuonyesha kurudi nyuma kwa mkojo.
  • Figo kupigwa picha maalumu (DMSA) ili kujua iwapo kuna makovu.

Matibabu

Ni muhimu kutibu hali hii ya mkojo kurudi ili kuzuia maambukizo na figo kuharibika. Matibabu hutegemea ukali wa hali hii, umri wa mtoto na dalili zilizopo.Kuna aina tatu za matibabu ya mkojo unaorudi ambazo ni dawa za antibayotiki,upasuaji na kukitia nguvu kilango cha yureta.Upasuaji na kuziba kilango hufanyiwa wagonjwa ambao hali yao ni mbaya zaidi na ambao hawasaidiwi na dawa. Matumizi ya dawa ndio chaguo la kwanza la tiba ya shida hii.

Hali ya mkojo kurudi ambayo ni kiasi (mild): Ikiwa hali hii haijazidi sana, huisha yenyewe mtoto afikishapo miaka mitano au sita. Watoto hawa hawahitaji upasuaji. Dawa za antibayotiki hutumiwa mara moja au mbili kwa siku, kila siku kwa muda mrefu ili kuzuia maambukizo. Dawa hizi za antibayotiki hutumiwa hadi mtoto afikishapo miaka mitano .Kumbuka dawa hizi hazirekebishi hali hii. Dawa ambazo mara nyingi hutumiwa ni Nitrofurantoin na cotrimoxazole.

Upasuaji na tiba ya endoscopi inapendekezwa wakati kuna VUR kali au wakati matibabu na antibiotiki hayakufaulu.

Watoto wote walio na shida hii lazima wazingatie hatua za kuzuia maambukizo kama ilivyoelezwa awali na pia mkojo kutolewa mara kwa mara. Mkojo pia upimwe mara ili kujua kama kuna maambukizo. Kila mwaka apigwe picha (VCUG na ultrasound) ili kujua kama hali hii inapungua au la.

Hali ya mkojo kurudi ambayo ni kali (severe) : Hali hii ikiwa imezidi haiwezi kujirekebisha yenyewe na kwa hiyo watoto wenye hali hii huhitaji upasuaji au kilango cha yureta kuongezwa nguvu ya kujifunga.Upasuaji huzuia mkojo kurudi nyuma. Kufaulu kwa upasuaji huwa asilimia themanini na nane hadi tisini na tisa, (88 – 99%) yaani uwezekano wake kufaulu uko mkubwa.

Kukitia nguvu kilango cha yureta ni njia ya pili ambayo husaidia sana hali mbaya ya mkojo unaorudi nyuma.Faida za njia hii ya tiba ni kwamba si lazima mgonjwa alazwe hospitalini, huchukua kama dakika kumi na tano tu, haina hatari nyingi na mgonjwa hakatwi. Mgonjwa hudungwa sindano ya nusukaputi na kwa kutumia tyubu yenye mwangaza,dawa hutiwa kwenye kilango cha yureta, hudungwa pahali pale palipoadhirika na kilango sasa huweza kuzuia mkojo kurudi. Ufaulu kwa njia hii huwa kama asilimia themanini na tano hadi tisini. Huwa ni njia nzuri ya kutibu hali ya mkojo kurudi kwani huzuia haja ya kutumia dawa na shida za kuishi na hali hii kwa miaka mingi.

Baada ya matibabu: Watoto wote wenye hali hii wafuatiliwe na kuendelea kupimwa urefu,uzito,shinikizo la damu,mkojo na vipimo vingine vinavyohitajika.

Wagonjwa wa VUR lazima wafuatiliwe mara kwa mara hasa kuona msukumo wa damu (blood pressure), ukuaji wao, maambukizi ya mara kwa mara ya mfumo wa mkojo na kuona kama kuna uharibifu wa figo.

Je, ni lini mtoto anafaa kumwona daktari?

  • Mtoto akipata homa, kutetemeka, maumivu au kuwashwa anapokojoa, mkojo wenye harufu mbaya au damu.
  • Kichefuchefu au kutapika ambavyo vitamfanya kushindwa kunywa maji au dawa.
  • Kuishiwa na maji kwa sababu ya kutokunywa maji au/na kutapika.
  • Maumivu ya upande wa chini wa mgongo au tumbo.
  • Kukosa raha, kukosa hamu ya chakula au kuonekana mgonjwa mgonjwa.